Maujanja ya kutengeneza siagi ya karanga nyumbani

Na Lucy Samson
6 Feb 2023
Siyo lazima kununua siagi dukani, unaweza kutengeneza yako ukiwa nyumbani kwa njia rahisi.
article
  • Ni rahisi kutengeneza
  • Utakachohitaji ni blenda, karanga,mafuta chumvi na asali kiasi

Siagi ya karanga ni moja ya kiungo pendwa kinachotumika kunogesha vitafunwa, au kifungua kinywa wakati wa asubuhi.

Kwa wanafunzi hususani waliosoma shule za bweni watakubaliana na mimi kuwa siagi ya karanga inachangamsha mlo. Iwe wa asubuhi, mchana au jioni ilimradi tu kuongeza ladha kwenye chakula cha shuleni.

Licha ya umuhimu mkubwa wa kiungo hichi kwenye kunogesha mapishi ya 

nyumbani bado baadhi ya watu wanapata changamoto kutengeneza.

Kwa muda mchache tu makala hii itakufundisha hatua kwa hatua jinsi ya kutengeneza siagi ya karanga nyumbani.

Mahitaji.

  1. Karanga mbichi robo

2. Maji kiasi

3. Mafuta kiasi

4. Chumvi robo kijiko

5. Asali vijiko 2

Ukijumuisha Siagi ya karanga na mlo wako wa asubuhi, unaweza kujipatia vitamin aina nyingi ikiwemo Vitamin E, B6, madini chuma na protini. Picha|People Blog.

M

Maandalizi

Hatua ya kwanza kwenye uandaaji wa siagi hii ni kuchambua karanga na kuondoa uchafu wote unaoweza kuwepo kisha zioshe na uziache zichuje maji.

Baada ya maji kuchujika hatua inayofuata ni kuzikaanga karanga. Utaanza kwa kuwasha jiko na kuweka sufuria utakayotumia kukaangia karanga.

Sufuria ikipata moto mimina karanga na uzipike/zikaange bila kutumia mafuta  kwa moto mdogo mdogo mpaka ziive.

Zikiiva vizuri epua na uzitoe maganda ikiwa unapendelea siagi nyeupe au uziache hivyo hivyo na maganda yake ikiwa unapendelea karanga zenye rangi.

Hatua inayofuata ni ya kuzisaga mpaka zitakapobadilika na kuwa siagi.

Faida ya kuengeneza siagi ya karanga nyumbani ipo kwenye kuamua uzito na ulaini unavyotaka siagi yako iwe.Picha|Cook at home mom

Fanya haya

Utahitaji blenda inayosaga vitu vikavu (heavy duty blender) ikiwa hauna unaweza kutumia kisagio kidogo cha blenda ya kawaida (grinder) ambacho mara nyingi hutumika kusagia vitu vikavu.

Ukishaandaa kifaa chako cha kusagia mimina karanga kiasi na uanze kusaga. Pumzisha blenda kila baada ya dakika tatu mpaka karanga zisagike na kubadilika kuwa siagi.

Kila baada ya dakika tatu funua blenda na ugeuze kwa kijiko karanga zinazogandia kwenye blenda ili kuruhusu karanga zote kusagika.

Karanga zikianza kuwa laini ongeza vijiko kadhaa vya mafuta ikiwa siagi yako ni kavu.

Saga mpaka upate mchanganyiko mlaini na uzito unaotaka. Ukiona ni mzito sana ongeza mafuta mpaka utakaporidhishwa na uzito wa siagi yako.

Ongeza chumvi na vijiko viwili au vitatu vya asali kama unapendelea kisha usage tena ichanganyike.

Mpaka hapo siagi yako itakuwa tayari unaweza kuiweka kwenye kontena safi lenye mfuniko na ukaitumia mpaka wiki tatu bila kuharibika.

© Copyright 2021 JikoPoint by Nukta Africa