Ijue namna ya kupika tambi zisizohitaji mboga

Na Maria Acley
25 Jan 2022
Mapishi ya tambi ni rahisi na yanatumia muda na mahitaji machache. Hata gharama zake siyo kubwa.
article
  • Ni chakula kinachotumia mahitaji machavhe.
  • Nyana, mayai, kitunguu, karoti ni viungo vya nyongeza kwenye pishi hili.
  • Chakula hiki hakichukui zaidi ya dakika 45 kuandaa.

Wakati mwingine mtu unakuwa umechoka na haupendi kupoteza muda jikoni. Mo wa chapchap unakuwa ni wazo zuri.

Moja ya vyakula vya haraka ni tambi za mayai yaani ‘pasta’ zenye mayai ndani yake. Zinapikwaje? Jibu lako lipo hapa. 

Mlo huu ni rahisi kuandaa na haukuchukui zaidi ya dakika ishirini chakula kinakuwa tayari mezani.

Tunahitaji vitu vichache tu na visivyo na gharama kutengeneza pishi letu.

Vitu hivyo ni pamoja na tambi, mayai na nyanya. Mahitaji mengine ni kama yanavyoonekana kwenye picha ifuatayo.

Maandalizi.

Chukua tambi ulizoandaa na uzikatekate. Kwa tambi za ndefu kama za “Mo”, mimi huwa nazikata mara tatu.

Ili kurahisisha na kutumia muda mchache jikoni unaweza kuanza kuchemsha maji huku ukiendelea na maandalizi ya viungo vingine.

Injika sufuria jikoni weka maji kiasi yatakayotosha kuchemsha tambi kisha ruhusu maji yachemke. 

Saga nyanya zako vizuri kisha ukate vitunguu kwa style unayoipenda wewe. Ukimaliza yote hayo, maji yako yatakuwa yamechemka.

Weka tambi ulizoziandaa kisha weka sukari vijiko vitatu vya chakula.

Kumbuka tunapika tambi nusu pakti hapa kwa kuwa mimi siwezi kumaliza mfuko wote. Kama umepika pakti nzima, utakadiria kiasi cha sukari kadri ya mapenzi yako.

Kama  sio mpenzi wa sukari unaweza kutumia chumvi kidogo. Acha tambi zako ziive huku ukiendelea kuandaa viungo vingine.

Andaa karoti kwa kuisaga, katakata hoho kwa maumbo mazuri yatakayovutia kwenye chakula. Hatua inayofuata ni kupasua mayai yako kwenye bakuli, weka chumvi kidogo na uyakorogoke vizuri kuchanganya chumvi na mayai.

Tambi za mayai ni rahisi kupika na hazihitaji mboga. Picha| Gazeti la Mtandao.

Tukarangize msosi wetu.

Kama una majiko mawili itapendeza zaidi lakini ukiwa na moja hakijaharibika kitu. Tunaweza kutumia hilo hilo moja kufanya maajabu.

Anza kwa kutazama tambi zako kama zimeiva. Kama ndiyo, ziepue na uzitoe kwenye maji kama maji hayakukauka lakini kama maji yamekauka ziache humo humo kwenye sufuria.

Injika sufuria nyingine jikoni na uweke mafuta ya kupikia vijiko viwili au vitatu vya chakula, weka vitunguu maji kisha uvikaange mpaka viwe na rangi ya kahawia.

Vitunguu vikiwa tayari, kwenye sufuria hilo ongeza karoti yako uliyoisaga mapema na uikaange kwa muda wa dakika moja, ongeza nyanya kwenye mchanganyiko huo na uipike mpaka uanze kuona imeiva vizuri na mafuta yaonekane juu ya nyanya.

Weka mchanganyiko wa mayai na chumvi tuliouandaa kabla kisha ukoroge mpaka mayai yaive vizuri.

Baada ya hapo chukua tambi zako ulizochemsha na uongeze kwenye mchanganyiko wa vikorombwezo vyote.

Koroga vizuri ili tambi  pamoja na vikorombwezo vyote vichanganyike vizuri, weka hoho na ufunike chakula chako kwa muda wa dakika nne tu.

Funua chakula chako, kigeuze kwa kukichanganya. Bila shaka pua zako zimeanza kunusa harufu nzuuuri. Hiyo ni taarifa kuwa chakula kimekwiva bwana. Pakua msosi wako na uenjoy.

Kwa mapishi ya misosi mitamu inayochukua muda mchache, JikoPoint tupo kwa ajili yako.

© Copyright 2021 JikoPoint by Nukta Africa