Wali ni miongoni mwa vyakkula maarufu vinavyopikwa mara kwa mara katika nyumba nyingi nchini Tanzania.
Umaarufu wa chakula hicho huonekana zaidi katika matukio muhimu ikiwemo sherehe, ambapo hupikwa wa aina mbalimbali ili kuvutia wageni.
Licha ya umaarufu wake, mapishi ya aina moja ya chakula hiki huchosha walaji hivyo unaweza ukatumia karoti kuongeza ladha na ubunifu katika chakula chako.
Mbali na kuongeza ladha karoti zinaongeza vitamini A, zenye manufaa kwa macho, ngozi na afya ya mwili kwa ujumla. Hivyo fuatana nami mpaka mwisho ujjifunze jinsi ya kuandaa chakula hiki.
Mahitaji
Vikombe 2 vya mchele safi
Karoti 2–3 kubwa, zilizosagwa vipande vidogo
Vijiko 2 vya mafuta ya kupikia
Kitunguu kimoja, kilichokatwa vipande vidogo
Kijiko 1 cha chumvi
Kitunguu swaumu punje 5
Maji ya moto/supu.

Hatua kwa hatua jinsi ya kuandaa
Anza kwa kuchambua na kuosha mchele vizuri chini ya maji baridi ili kuondoa uchafu kisha endelea na maandalizi mengine ikiwemo kukatakata vitunguu pamoja na kusaga karoti.
Washa jiko kisha bandika sufuria yenye mafuta ya kupikia kiasi, yakipata moto weka vitunguu maji, vikilegea kidogo ongeza kitunguu swaumu ikifuatiwa na karoti zilizosagwa na ukoroge kwa dakika mbili au tatu.
Baada ya karoti kulegea ongeza mchele pamoja na chumvi na uchanganye vizuri kabla ya kuongeza maji ya moto au supu na kufunikia kwa daika 10 hadi 15 kw moto mdogo mdogo ukisubiri uive.
Kama wewe ni mpenzi wa nazi unaweza kuiongeza katika hatua hii ili kuongeza ladha zaidi na mvuto wa msosi wako.
Baada ya muda huo kupita geuza chakula chako na ikiwa kipo tayari unaweza kuepua na kuweka mezani ikisindikizwa na mboga yoyote uipendayo.