Ikiwa unatafuta kinywaji kuongeza joto, kilichojaa faida za kiafya na ladha ya kipekee, basi chai ya tangawizi na asali pamoja na limao ni chaguo bora kwa ajili yako.
Tovuti ya masuala ya afya ya Healthline inabainisha kuwa unywaji wa kinywaji hiki husaidia mmeng’enyo wa chakula, kusafisha utumbo, kuongeza joto mwilini, kupunguza shinikizo la damu,kutibu magonjwa kama mafua, kichwa kuuma, kichefuchefu na maumivu ya viungo.
Si hayo tu, unywaji wa kinywaji hiki unaweza kuupa mwili joto katika kipindi cha baridi au kwa wakazi wa maeneo huwa kwenye hali ya ubaridi mwaka mzima.
Ili kupika kinywaji hiki utahitaji, asali, limao pamoja na tangawizi hivyo njoo tupike pamoja.
Namna ya kuandaaa
Ili kuandaa chai hii hatua ya kwanza ni kuosha mahitaji yako hususan limao na tangawizi kisha menya maganda ya tangawizi na ukate vipande vidogo vidogo bila kusahau kukamua juisi ya limao kisha vitenge pembeni.
Hatua inayofuata ni kuandaa chombo utakaochokitumia kisha weka asali kiasi pamoja na tangawizi ambayo umeiandaa awali.
Baada ya hapo katika mchanganyiko huo wa asali na tangawizi 0ngeza vipande viwili vya limao vilivyokatwa kisha weka juisi ya limao uliyoiandaa.
Ongeza maji ya moto yaliochemka na chai yako itakuwa tayari kwa kunywa.