Mara nyingi wapishi wamezoea kutumia mafuta kama moja ya kiungo kinacholeta ladha kwenye chakula. Lakini leo naomba tujaribu kupika mboga aina ya samaki bila kutumia mafuta yaani mboga na nazi pekee.
Jikoni kwetu leo mboga yetu leo ni samaki ambaye tutaenda kumuandaa kwa ajili ya chakula cha jioni au mchana.
Mahitaji ni samaki wabichi au wakavu, nyanya maji, kitunguu maji, karoti, nyanya chungu, bamia, ndimu au limao, nazi kubwa moja na chumvi.
Baada ya kuandaa viungo hivi, kinachofuata ni kuchukua Samaki wakavu loweka kwenye maji ya moto hadi walainike kama ni samaki wabichi wachemshe au wakaange kwanza.
Wakati unaloweka au kuwachemsha hakikisha umewamiminia limao na tangawizi kisha waache ndani ya dakika 15. Baada ya hapo katakata kitunguu na nyanya kisha saga karoti.
Anza kupika pishi lako
Bila kuweka mafuta bandika sufuria jikoni kisha mimina hivyo viungo na samaki kwa pamoja ongeza maji kidogo acha vichemke kisha kamulia ndimu au limao.
Wakati hivyo viungo vikiwa jikoni vinachemka weka bamia, nyanya chungu na samaki kisha changanya. Mimina tui la pili la nazi lile jepesi kiasi kisha bila kufunika acha viive.
Baada ya tui la pili kukauka weka tui la kwanza lile zito na mimina chumvi kiasi changanya acha mboga ichemke hadi iive. Baada ya hapo mboga itakuwa tayari kwa chakula unaweza kuitumia kwa ugali, wali au ndizi za kuchemsha.